Geita.
Juhudi za kuwatafuta wachimbaji wadogo zimeonyesha dalili nzuri baada
ya kufahamika kuwa wapo hai, lakini bado wakiwa wamefukiwa ardhini.
Jana, watu hao walituma ujumbe uliotaja majina yao na idadi kwamba wako 15, tofauti na 14 kama ilivyokuwa ikiripotiwa awali.
Taarifa kutoka mgodini zilizolifikia gazeti hili zilieleza kuwa, baada
wachimbaji hao kugundulika kwa mara ya kwanza walipofikiwa na bomba,
walirudisha ujumbe kueleza idadi yao na kwamba walikuwa na njaa na kiu
hivyo wakaomba watumiwe sigara, soda na maji.
Akitoa taarifa kwa Naibu Waziri wa Nishati, Medadi Kalemani, mmoja wa
watu waliopo katika timu ya uokoaji, Felix Adolf alisema licha ya maombi
hayo, ilishauriwa kuwa watu hao waliofukiwa watumiwe maji ya glucose
yanayochanganywa na timu ya madaktari iliyopo hapo.
Wachimbaji hao waliofukiwa na kifusi cha udongo kwa zaidi ya siku tatu
sasa katika Mgodi wa RZ mkoani Geita, wamekuwa wakiwasiliana kwa kutumia
bomba la kuchimbia maji.
Katibu wa wachimbaji wadogo katika Mkoa wa Geita, Golden Hainga alisema
jana kuwa kazi ya kuchimba ili kuingiza bomba la kuwapelekea maji na
chakula wachimbaji hao walioko chini, ilifanikiwa na waligonga bomba
hilo kuashiria kuwa wako hai.