Profesa Ibrahim Haruna Lipumba alizaliwa 6 Juni 1952 katika Kata ya Ilolangulu Wilaya ya Uyui katika Mkoa wa Tabora nchini Tanzania (Tanganyika wakati huo).
Elimu
Alipata elimu yake ya msingi katika Shule ya Wamishenari wa Sweden kuanzia mwaka 1959 hadi 1962, kisha akaenda Shule ya Msingi L.A Upper mwaka 1962 hadi 1966. Baadae alijiunga na Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora (Tabora Boys) kuanzia mwaka 1967 hadi 1970. Alipohitimu hapo, mwaka 1971 na 1972 alikuwa Shule ya Sekondari Pugu na alifaulu kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1973 na alihitimu Shahada ya Uchumi mwaka 1976.
Prof Lipumba alipata Shahada yake ya Umahiri (Masters Degree) katika Uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1978 ndipo akajiunga na Chuo Kikuu cha Stanford kilichopo California nchini Marekani kwa ajili ya Shahada ya Uzamivu (PhD) katika uchumi aliyotunukiwa mwaka 1983.
Ajira
Prof. Lipumba ameshika nyadhifa mbalimbali. Amewahi kuwa Mhadhiri katika chuo nchini Marekani na Tanzania pia. Amefanya kazi na makampuni mbalimbali kuhusu masuala ya uchumi na pia mwishoni mwa miaka ya 1980 na mwanzoni 1990, alikuwa mshauri wa masuala ya uchumi katika Serikali ya Uganda.
Maisha ya Siasa.
Prof. Lipumba amekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) tangu mwaka 1995 hadi sasa (kwa sasa kuna mvutano juu ya uhalali wake kama Mwenyekiti wa CUF). Amegombea katika chaguzi zote tangu kuwanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi isipokuwa uchaguzi wa mwaka 2015.
Maisha nje ya siasa
Prof. Lipumba alikuwa mchezaji mzuri wa mpira wa miguu akiwa sekondari, lakini alilazimika kustaafu kucheza baada ya kupata majeraha ya goti. Ni shabiki wa timu ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars) na klabu ya Arsenal ya nchini Uingereza. Prof. Lipumba ameoa.