Brazzaville, Gabon. Timu ya Taifa ya Cameroon ‘Simba Wasiofugika’
imetinga nusu fainali ya mashindano ya Afcon baada ya kuitoa timu ya
Taifa ya Senegal ‘Simba wa Teranga’ kwa jumla ya mikwaju ya penalti 5-4.
Cameroon imeungana na Burkina Fasso ambayo ilikuwa ya kwanza kutinga nusu fainali baada ya kuifunga Tunisia 2-0.
Nyota anayeichezea Liverpool, Sadio Mane ndiye aliyeiponza Senegali
kwani penalti yake aliyoipiga imepanguliwa vema na kipa wa Cameroon,
Fabrice Ondoa.
Dalili za Ondoa kumnyima Mane usingizi usiku huu zilionekana ndani ya
dakika 90 za mchezo kwani licha ya straika huyo wa Senegal kutafuta
goli, kipa huyo alilinda lango lake kikamilifu na hatimaye mchezo
umemalizika kwa timu hizo kutoka suluhu ya 0-0.
Hata baada ya kuongezwa kwa dakika nyingine 30, Simba hao wa milima ya
Teranga na Simba Wasiofugika walishindwa kufungana hadi walipoingia
kwenye hatua ya mikwaju ya penalti.
Miaka 15 iliyopita, miamba hiyo ya soka ilikutana katika hatua ya
fainali, Cameroon iliishinda Senegal kwa penalti 3-2 na kutwaa ubingwa
wa AFCON kwa mara ya nne huko Bamako, Mali.