» » Polisi kuporwa silaha ni aibu-Kamanda Siro

ILI UPATE HABARI ZETU KWA URAHISI BOFYA HAPA KUINSTAL APPLICATION YA MZALENDO HURU KWENYE SIMU YAKO


Dar es Salaam. Kamanda wa Kanda Maalumu ya Kipolisi ya Dar es Salaam, Kamishna Simon Sirro amesema kitendo cha askari kunyang’anywa silaha na majambazi ni aibu na fedheha kwao na Jeshi la Polisi, akisema madhara yake yanaweza kuwa makubwa kwa jamii.
Kamanda Siro pia amesema tukio la uvamizi wa kituo cha polisi cha Stakishari jijini Dar es Salaam na silaha kuporwa lilikuwa fedheha kwa Jeshi la Polisi, lakini akabainisha kuwa halikuwa na viashiria vya ugaidi bali ujambazi.
Kamanda Siro, ambaye wakati wa tukio hilo alikuwa Msaidizi wa Kamishna wa Polisi wa Kanda ya Dar es Salaam, amesema hayo katika mahojiano maalumu na Mwananchi yaliyofanyika wiki iliyopita.
Kauli ya Kamanda Siro imekuja wakati nchi ikiwa kwenye mapambano makali na watu wanaodhaniwa kuwa majambazi ambao wana silaha kali, kiasi cha kustahimili kupambana na polisi kwa zaidi ya saa kumi.
Akijibu swali kuhusu matukio ya askari kunyang’anywa silaha yaliyotokea kwa wingi mwaka jana, Kamanda Siro alisema ‘‘Yalikuwa aibu kwa askari na Jeshi la Polisi kwa ujumla. Ni aibu kubwa,” alisema Kamanda Siro.
“Fikiria wewe ni kiongozi, unapata habari kwamba askari amenyang’anywa silaha, itakuwaje. Ni aibu kubwa kwa Jeshi la Polisi.
“Na kuna athari mbili za kunyang’anywa silaha. Kwanza silaha hiyo inaweza kutumika katika matukio ya uhalifu, lakini pili hujui itatumikaje. Inaweza kutumika kwenye vikundi hatari. Silaha za Jeshi la Polisi ni zile ambazo haziuzwi madukani.”
Alipoulizwa alijisikiaje wakati watu wasiofahamika walipovamia kituo cha Stakishari kilichopo Ukonga wilayani Ilala Julai 13 mwaka jana, Kamanda Siro alisema ilikuwa fedheha kwa Jeshi la Polisi.
“Unapokuwa kiongozi halafu silaha ikichukuliwa, huwa ni tatizo kwetu na lazima itakupa shida,” alisema mkuu huyo wa zamani wa operesheni za Jeshi la Polisi.
“Ila namshukuru Mungu hatujapata changamoto kubwa.”
Alisema wakati huo alikuwa msaidizi wa Kamanda wa Polisi wa Kanda ya Dar es Salaam, Suleiman Kova na wakati wa tukio alikuwa likizo.
“Lakini niliitwa kazini kutokana na tukio hilo. Lakini tulibaini baadaye kuwa ulikuwa ni ujambazi.”
Tukio la Stakishari lilikuwa miongoni mwa matukio kadhaa ya uvamizi wa vituo vya polisi mwaka jana.
Kabla ya uvamizi wa Stakishari, majambazi walivamia na kukiteka kituo cha polisi cha Ikwiriri kilichopo tarafa ya Ikwiriri, wilayani Rufiji, mkoani Pwani na kuwaua askari wawili, kupora silaha saba na kisha kulipua bomu. Pia walivamia kituo kidogo cha polisi cha Mngeta mkoani Morogoro na kupora bunduki aina ya SMG na magazini moja yenye risasi 30.
Pia, majambazi walivamia kituo kidogo cha Mkamba mkoani Pwani na kusababisha kifo cha askari mmoja na mgambo. Pia, walipora silaha tatu aina ya shot gun tatu, SMG mbili na magazini 30 kila moja ambazo zilikuwa kwenye ghala la muda zikisubiri kupelekwa kwenye kituo kikubwa kwenye ghala kuu la silaha.
Pia, majambazi walivamia kituo kikuu cha polisi cha wilayani Bukombe mkoani Geita mwaka juzi ambako askari wawili waliuawa na kujeruhi wengine watatu.
Akizungumzia hali ya kazi tangu ateuliwe kuongoza Kanda ya Dar es Salaam, Siro alisema Jeshi la Polisi imepambana na watu takribani 100 waliokuwa wakilitikisa jiji kwa uhalifu na ujambazi na kufanikiwa kuwadhibiti.
Amesema kuwadhibiti watu hao hakuna maana kuwa polisi imemaliza kabisa matukio hayo, bali inaendelea kupambana kuhakikisha Jiji linakuwa katika hali ya usalama wakati wote, huku akieleza mambo saba yaliyofanyika kufanikisha mkakati wake huo.
Sirro alisema watu hao 100 walikuwa wakipora raia waliokuwa wanatoka benki, kuvamia nyumba za watu na kupora na kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya.
Sirro, ambaye aliteuliwa na Rais John Magufuli Februari 15 kuchukua nafasi ya Kova aliyestaafu, alisema: “Tangu nimekaa hapa tumepambana na watu wengi sana, ni watu zaidi ya 100 na hata bunduki tulizokamata ni nyingi.
“Wapo wanaotangulia mbele ya haki na hao ni wengi maana walipambana na polisi. Huwa nawauliza askari mtu mwenye bunduki unamkamataje? Stahiki yake tunajua sisi tulioajiriwa kwa kazi hii.”
Kamanda huyo anayezungumza kwa kujiamini, amewahi kuwa Kamanda wa Polisi katika mikoa ya Tanga, Mwanza na Shinyanga.
Kamishna Sirro alisema bunduki zilizokuwa zikitumiwa na baadhi ya majambazi hao ni za kivita kama SMG, ambazo alisema zinapokamatwa wahusika hufikishwa mahakamani na mahakama hutoa amri silaha hizo kurejeshwa serikalini au kuteketezwa kama zitakuwa zimeharibika.
ILI UPATE HABARI ZETU KWA URAHISI BOFYA HAPA KUINSTAL APPLICATION YA MZALENDO HURU KWENYE SIMU YAKO

About Mashak

About Mzalendo Huru Staff:

Send us your articles, questions, feedback, suggestions, press releases and all others to Whats app on +255657905751
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post