Dar es Salaam. Taasisi
ya Kigoda cha Mwalimu Julius Nyerere imetoa tuzo kwa watu watatu
walioonyesha kuziishi falsafa za Rais huyo wa kwanza wa Tanzania. Tuzo
hizo zilizotolewa kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwake miaka minane
iliyopita, lengo likiwa ni kutunza na kuendeleza yote aliyosimamia
Mwalimu Nyerere.
Tuzo
hizo zilitolewa kwa Mwanzilishi wa Vikoba, George Swevetta, aliyekuwa
Mkuu wa Sekondari ya Weruweru, Dk Maria Kamm na marehemu Mtimbanjao
Milinga, aliyeanzisha vijiji vya ujamaa kabla Serikali kufanya hivyo.
Akiwaelezea
washindi hao, mshereheshaji wa dhifa hiyo, Profesa Penina Mlama alisema
ni jambo la heshima kuwa na watu wanaoweza kujitoa kwa ajili ya
Watanzania kama alivyofanya Mwalimu Nyerere.
Swevetta
alizianza harakati za kuwajengea uwezo kiuchumi watu wenye kipato cha
chini hasa wanawake akiwa visiwani Zanzibar mwaka 2000. Baada ya miaka
miwili, jitihada hizo zilizokuwa na mafanikio alizianzisha pia bara.
