Polisi wakimkamata mfuasi wa Chadema aliyekuwa akishiriki mkutano wa
hadhara kwenye viwanja vya DCT wilayani Kahama, Shinyanga wiki
iliyopita. Mkutano ulivunjika baada ya polisi kupiga mabomu. Picha ya
Maktaba
Jeshi
la polisi limesambaratisha mkutano wa hadhara wa Chama cha Demaokrasia
na Maendeleo (Chadema) kwa kupiga mabomu ya kutoa machozi.
Kitendo
hicho kimefanyika hivi karibuni katika mji wa Kahama mkoani Shinyanga
ambako wafuasi wa chama hicho wakiongozwa na mwenyekiti wao, Freeman
Mbowe walitaka kufanya mkutano wa uzinduzi wa Operesheni ya Okoa
Demokrasia.
Chama
hicho kilitaka kupaza sauti kupinga hatua wanazodai zinachukuliwa
katika kuikandamiza demokrasia nchini na kuwanyima nafasi wapinzani.
Polisi
waliingia katika eneo hilo la mkutano na kuanza kupiga watu huku
wakifyatua mabomu ya machozi na kuusambaratisha mkutano huo.
Ilidaiwa
kuwa baadhi ya watu waliopinga kitendo hicho walirusha mawe kwa polisi,
lakini haikuwasaidia kuweza kufanya mkutano huo.
Tukio hili linatokea wakati katika nchi ya jirani ya Kenya kuna maandamano ya wafuasi wa upinzani kila Jumatatu.
Wafuasi hao wa upinzani wa Kenya wanadai Makamishna wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Kenya waondolewe madarakani.
Wafuasi
hao kutoka upinzani wanadai kwamba maofisa wa Tume ya Uchaguzi
wanakipendelea chama tawala kwa hiyo hawataki wasimamie Uchaguzi Mkuu wa
Kenya utakaofanyika mwakani.
Serikali
ya Kenya ilijaribu kupiga marufuku maandamano hayo, lakini Mahakama Kuu
ya Kenya ilikataa na kuruhusu yaendelee na kuwataka Polisi wachukue
jukumu la kulinda amani.
Kimisingi
hiyo ndiyo kazi ya polisi ya kulinda amani ili wananchi wapate fursa ya
kutoa dukuduku lao kwa kufanya maandamano na mikutano ya hadhara kwa
njia ya amani.
Polisi wapiga marufuku
Katika
hatua ya kushangaza Jeshi la polisi Tanzania hivi karibuni limepiga
marufuku maandamano na mikutano ya hadhara yote ya vyama vya siasa.
Polisi
walitangaza hatua hiyo wakidai kwamba kuna viashiria vina vyoonyesha
kutatokea uvunjifu wa amani iwapo mikutano ya hadhara itafanyika. Jeshi
hilo lilieleza kuwa kuna hali inaonyesha kuwa pande mbili
zinazohasimiana zinaweza zikaleta vurugu.
Polisi
walieleza kuwa wanazuia mikutano hiyo ya hadhara kwa madai kuwa baadhi
ya vyama vya siasa vina nia ya kuwaeleza wananchi wasitii sheria za
nchi.
Katika
mazingira ya Tanzania hakuonyeshi kwamba kuna dalili yoyote ya kutokea
uvunjifu wa amani kwa vile hali ni ya amani na utulivu isipokuwa mauaji
ya hapa na pale ambayo hayahusiani na sababu za kisiasa. Ni jukumu la
polisi kuhakikisha kuwa ni lazima wimbi hilo la mauaji ya wananchi wasio
na hatia, lakini jambo hilo halina uhusiano na mikutano ya vyama vya
siasa.
Kazi
ya Jeshi la polisi siyo kupiga marufuku kwani maandamano na mikutano ni
utashi wa vyama vya siasa na wao haiwahusu, bali jukumu lao ni kulinda
amani ili ifanyike bila madhara yoyote.
Ni makosa makubwa kwa polisi kujipa jukumu la wenyewe ndiyo waamuzi wa lini vyama vya siasa vifanye mikutano ya hadhara.
Hawana
uhalali wa kupiga marufuku maandamano na mikutano ya hadhara ya vyama
vya siasa, bali jukumu lao ni kutoa ulinzi kuhakikisha kwamba
linafanyika kwa njia ya amani na utlivu.
Kama
polisi inaona kuna watu wana nia ya kuleta vurugu kwenye mkutano wa
chama fulani wao jukumu lao ni kuwadhibiti hao waleta vurugu na siyo
kupiga marufuku mikutano.
Kupiga
marafuku mikutano au na maandamno ya vyama vya siasa ni kuizuia
demokrasia kuchukua nafasi yake na ni kinyume cha haki za binaadamu.
Watu
wowote wale wakitaka kuandamana au kufanya mkutano wa hadhara hata kama
wanataka kubishana kati ya kuku na yai ni nani aliyeanza wana haki ya
kufanya hivyo na polisi kazi yao ni kuwalinda tu.
Kazi ya polisi siku zote ni kulinda amani, lakini siyo kutoa ruhusa ya kufanyika maandamano au mikutano ya hadhara.
Ni mtihani wa demokrasia
Uamuzi
wa aina hii wa polisi unaleta taharuki katika nchi ambayo haikupaswa
kuwapo kwani wananchi wanatakiwa wawe huru kutoa maoni yao almuradi
hawavunji Sheria.
Siyo
jambo la busara hata kidogo kwa polisi kuchukua hatua za namna hii
ambazo zinakwaza demokrasia ambayo kwa Tanzania bado ina safari ndefu.
Hakuna
haja ya kuwadhibiti watu wasifanye maandamano na mikutano ya hadhara
kwa kisingizio chochote kile kwani kufanya hivyo ni ukiukwaji mkubwa wa
demokrasia.
Tanzania
itakuwa nchi ya kushangaza kama kila kitu kinapigwa marufuku hata
matangazo ya moja kwa moja kwa njia ya Televisheni ya Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania.
Sasa
badala ya kupiga marufuku matangazo hayo ya Bunge sasa marufuku
inakwenda katika vyama vya siasa hasa vya upinzani ili visipate nafasi
ya kuwasiliana na wanachi.
Mtindo
wa polisi kuvunja maandamano kwa nguvu kwa kutumia mabomu ya machozi na
silaha nyingine ni wa hatari kwani kuna siku wananchi nao watachoka
kufanyiwa vitendo hivyo na watakuja juu.
