» » MC-MKONGWE : Chama cha Mapinduzi kitabadilika na kuacha mazoea?

ILI UPATE HABARI ZETU KWA URAHISI BOFYA HAPA KUINSTAL APPLICATION YA MZALENDO HURU KWENYE SIMU YAKO



Swali hili lipo kwenye mawazo ya wananchi wengi na hata baadhi ya viongozi wenyewe kwenye Serikali Kuu. Viko viashiria kadhaa ambavyo vinaonyesha hali ya ‘figisufigisu’ kutokana na matamko ya baadhi ya viongozi wenyewe wa CCM hasa kutokana na mazoea waliyokuwa nayo ya kiuongozi.
Viongozi wengi ni walewale kwenye idara zilezile ndani ya chama, tena wameshikwa na butwaa kutokana na aina ya uongozi wa Rais John Magufuli ambao unaishushua CCM kwa maovu yote yaliyotendeka nchini.
Yawezekana baadhi ya wanajamii wakaona kuwa ufisadi unaopelekea majipu kutumbuliwa ni wa viongozi wa Serikali Kuu, lakini hebu tujiulize Serikali hiyo iliundwa kutokana na chama kipi? Jibu la moja kwa moja na sahihi ni Chama cha Mapinduzi (CCM). Butwaa linazingira nafsi za wananchi wengi wanapofikiria juu ya mwingiliano wa uamuzi kati ya Rais Magufuli na utashi wa kimazoea wa uongozi wa CCM. Yawezekana pia, wananchi na hata wafanyabiashara wakasema kasi ya Rais Magufuli kiutendaji huenda itapungua.
Kukosolewa kwa Rais Magufuli
Wapo baadhi ya wanajamii, wasomi na viongozi wastaafu ambao kwa namna tofauti mara kadhaa wakionekana wazi kabisa kuukosoa uongozi wa Rais Magufuli na hata kutilia shaka ya udhaifu wa utendaji kazi wa viongozi aliowateua.
Wapo baadhi yao ambao wanaonekana dhahiri wanatenda kazi kwa woga au shaka na kutojiamini. Pia, wapo ambao hawana uhakika na kesho yao.
Inadhihirishwa hata na majipu makubwa ambayo yanatumbuliwa na Rais kwenye wizara zao, ilhali wao wenyewe wapo au wamekaa kimya. Ni hofu au bado wana mawazo ya mfumo-sera wa kubebana na kulindana ndani ya CCM?
Zipo pia fikra za wanajamii na viongozi kuwa labda taarifa zote za uozo uliotendeka hapa nchini zinalengwa kupelekwa moja kwa moja kwa Rais Magufuli.
Hili limezuka kutokana na kutojiamini kwa baadhi ya watendaji wakuu kutokuwa na ujasiri wa kutoa uamuzi mgumu; ama kuendeleza sera ya CCM ya kuoneana aibu.
Kutokana na kasi ya kiutendaji ya Rais Magufuli ni dhahiri kuwa Serikali kuu imekuwa ni mwiba mkali kwa CCM ambayo ndiyo iliyoiunda Serikali zote zilizopita, bali Serikali za miongo mitatu iliyopita ndizo zilizotia fora kwa kuwasononesha wananchi. Serikali ya Rais Jakaya Kikwete ndiyo inayoongoza kwa kashfa tele ambazo zilifumbiwa macho, sasa zinatumbuliwa kama majipu.
Chimbuko jema la kila jambo la kiuongozi ni kuanzia kwenye shina lake na shina la kila serikali ulimwenguni hutokana na chama cha siasa kilichochaguliwa na wananchi, kiuongozi Serikali hiyo kama chama kitakuwa na utendaji makini na adilifu.
Rushwa sugu nchini
Kitendo hiki kiovu kiitwacho ‘rushwa’ kimeota mizizi katika sekta mbalimbali za kiofisi, hata kwenye maeneo ya kijamii nchini kote.
Kwenye kila huduma uitakayo utakuta imezingirwa na viashiria vya kuombwa rushwa ambayo iko katika majina tofauti. Hivi karibuni Rais Magufuli alifuatana na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia Rushwa (Takukuru) kwenye kongamano la makandarasi nchini kwa sababu maalumu.
Hii ni ishara inayoonyesha ni jinsi gani ambavyo Rais anavyoichukia rushwa na kuwa na nia thabiti ya kuondosha ama kuipiga vita ya aina yoyote nchini.
Rais Magufuli alisema tena kwa msisitizo “makandarasi msichukue rushwa na mtoe taarifa kwa yeyote anaewaomba rushwa hata kwenye bodi za kutoa tenda za kazi zenu; ndiyo maana nimemleta mkurugenzi huyu mumpe taarifa zozote mlizonazo’.
Jambo hili linalokaziwa na Rais linawapa hofu kubwa watendaji waovu, hata baadhi ya viongozi waliouzoe mfumo mchafu uliozoeleka wa kufumbia macho matendo hayo.
Najua ni kazi ngumu hasa kwa baadhi ya viongozi wetu wengi wa nchi za Afrika ama za ulimwengu wa tatu. Nyingi zimezama kwenye wimbi la uovu huo-rushwa na ufisadi wa kila aina na nchi nyingine maovu hayo yanaongozwa na viongozi waku wenyewe, kujilimbikizia utajiri usiolezeka.
Rais Magufuli anahitaji kushirikiana na mawaziri wake, watendaji wakuu, watoa huduma mbalimbali pia, wananchi kuipiga vita tabia hii ovu. Ni kazi inayohitaji uwajibikaji wa kila mwanajamii kwa nia ya dhati; vinginevyo itachukua muda mrefu kutoweka ama kupungua ipasavyo.
Rai yangu, wana siasa ambao wananchi wamewapa kura zao wawe wawakilishi wa majimbo yao, wajinasue wenyewe kwenye mtego wa tamaa za kifisadi hasa wanapochangamana na baadhi ya wana siasa wanaowakuta kwenye dimbwi hilo la aibu ya rushwa.
Wapo wazoefu ambao katika kila kashfa wanatuhumiwa, na hao wadau wao kwa majina tofauti kama ‘wawekezaji ama wafanyabiashara’ na hata wana ukoo wa baadhi ya viongozi ndio waliotufikisha katika ‘uozo’ unaolitesa taifa letu.
ILI UPATE HABARI ZETU KWA URAHISI BOFYA HAPA KUINSTAL APPLICATION YA MZALENDO HURU KWENYE SIMU YAKO

About Mashak

About Mzalendo Huru Staff:

Send us your articles, questions, feedback, suggestions, press releases and all others to Whats app on +255657905751
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post