» » HOJA YANGU : Turejee mifumo wa kiintelijensia ya Mwalimu Nyerere

ILI UPATE HABARI ZETU KWA URAHISI BOFYA HAPA KUINSTAL APPLICATION YA MZALENDO HURU KWENYE SIMU YAKO


Taifa linapita katika wimbi zito la mauaji ya kikatili ikiwamo watu kuvamiwa na kuchinjwa kama kuku.
Matukio haya mapya ya watu kuvamiwa na kuchinjwa yameshuhudiwa hadi ndani ya nyumba za ibada kama ilivyotokea jijini Mwanza baada ya watu waliofunika nyuso zao kuvamia Msikiti wa Rahman, eneo la Mkolani na kuua watu watatu akiwamo Imam wa msikiti huo, Fereuz Ismail.
Katika Kijiji cha Sima, Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza, watu wasiojulikana walivamia familia ya Zakaria Mbata na kuwaua kwa kuwakata mapanga watu saba.
Miongoni mwa waliouawa ni pamoja na mama wa familia hiyo, Eugenia Phillipo, watoto wake watatu na wageni watatu wa familia hiyo. Wiki iliyopita mume na mke wakachinjwa na watu wasiojulikana waliovamia nyumbani kwao huko wilaya ya Butiama mkoani Mara.
Vumbi likiwa halijatulia, watu wasiojulikana wanaoaminika kujificha katika mapango ya Amboni mkoani Tanga wakavamia Kitongoji cha Kibatini mkoani humo na kuwaua kwa kuwachinja watu wanane kabla ya kupora vyakula dukani.
Mauaji ya aina hii ni mapya katika historia ya Taifa letu linalosifika duniani kuwa la amani na utulivu.
Zamani mauaji ya kukata watu kwa mapanga yalisikika mikoa ya Kanda ya Ziwa hasa Mwanza, Shinyanga, Geita na Simiyu yakihusishwa na imani za kishirikina.
Katika mauaji hayo ya kishirikina walengwa zaidi walikuwa ni vikongwe, hasa wanawake ambao ama walidaiwa kuhusika na vifo vya wana familia.
Suala la urithi na mgawanyo wa mali pamoja na migogoro ya mashamba au mipaka ya ardhi ilidaiwa kuwa miongoni mwa sababu za mauaji hayo.
Hata hivyo, aina mpya ya mauaji ya kukata mapanga na kuchinja yana sura tofauti.
Wauaji wanaua hadi watoto wanaokutwa kwenye eneo la tukio kama tulivyoshuhudia kule Sengerema.
Ingawa wahalifu wana mbinu na mikakati kadhaa ya kukwepa mikono ya dola wakati wa kutekeleza uhalifu wao. Nimeanza kutilia shaka uwezo wa kiintelijensia wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama.
Simaanishi kuwa vyombo vyetu havifanyi kazi. La hasha! Vinafanya kazi sana kwa sababu vimefanikiwa kudhibiti au kukabili matukio kadhaa ya uhalifu nchini.
Hata hivyo, nadhani uwezo wa kukusanya taarifa za kiintelijensia za vyombo vyetu na kuzifanyia kazi umepungua katika siku za hivi karibuni.
Yawezekana watendaji wa vyombo hivi hawatumii ipasavyo fursa za kupata taarifa za kiintelijensia na hivyo kuwapa mwanya wahalifu kupanga na kutekeleza uhalifu wao bila kubainika au uwezo wao katika mikakati ya kukabiliana nao umegota.
Tatizo lingine ninaloliona ndani ya vyombo vyetu ni kupuuza kwa makusudi au kwa bahati mbaya baadhi ya taarifa za kiintelijensia zinazofikishwa kwao na raia wema.
Baada ya mauaji ya Tanga, kuna taarifa kuwa vyombo vya dola viko imara na vinatenda kazi kwa haraka vinapopata taarifa zinazohusiana na masuala au matukio ya kisiasa.
Pia, yapo madai kuwa baadhi ya watendaji wa vyombo vya dola ama wanashiriki au wana uhusiano na makundi ya kihallifu. Watendaji hao wasio waaminifu wanadaiwa kuvujisha taarifa za kiintelijensia kwa wahalifu na hivyo kuwawezesha kukwepa mikono ya dola.
Kama Taifa, hatuwezi kuendelea kuvumilia hali hii ambayo siyo tu inaangamiza maisha ya wapendwa wetu, pia inachafua sura na sifa ya nchi yetu mbele ya dunia.
Ulianza ukataji viungo na mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi kwa imani za kishirikina ambao vumbi lake limeanza kutulia. Pamoja na mbinu zingine za kimafunzo, nadhani muda umefika turejee kwenye mfumo wa zamani wa enzi ya Serikali ya Awamu ya Kwanza chini ya Mwalimu Julius Nyerere ya taarifa za kiintelijensia kukusanywa kuanzia ngazi ya nyumba 10.
Mabalozi wa nyumba 10 warejeshewe nguvu za kisheria za kufuatilia, kubaini na kuorodhesha wageni na watu wote wanaoiongia na kuishi ndani ya maeneo yao kiutawala.
Hii itasaidia kubaini wageni wote na mienendo yao tofauti na sasa watu wanaweza kuishi mtaa mmoja kwa mwaka mzima bila kuonana wala kufahamiana nani ni nani na anafanya shughuli gani. Wapo watakaopinga wazo hili kwa madai kuwa siyo rahisi watu wote mtaani kujulikana shughuli zao. Lakini napenda kuhoji iliwezekanaje wakati ule, isiwezekane leo?
Ni suala la uamuzi na kuweka misingi ya sheria kufanikisha hili kwa faida na masilahi ya jamii yetu. Tuache siasa na mawazo ya kushindwa kabla ya kujaribu inapofika masuala ya msingi ikiwamo usalama wa raia na mali zake.
Kama kweli viongozi wetu wasema kwa dhati kuwa wanamuenzi Mwalimu Nyerere, basi waanze na hili la ulinzi na usalama kwa kurejesha mfumo imara na wa kisheria wa ulinzi na usalama kuanzia ngazi ya mabalozi wa nyumba 10 uliofanya Tanzania kuwa miongoni mwa mataifa yenye uwezo mkubwa kiintelijensia enzi hizo.
Vita dhidi ya uhalifu haviwezi kupiganwa na vyombo vya dola pekee vikafanikiwa. Umma lazima ushiriki kikamilifu kwa kutoa taarifa za kiintelijensia zitakazosaidia kunasa wahalifu na hiyo sharti ianzie ngazi ya chini kabisa ya nyumba 10.
ILI UPATE HABARI ZETU KWA URAHISI BOFYA HAPA KUINSTAL APPLICATION YA MZALENDO HURU KWENYE SIMU YAKO

About Mashak

About Mzalendo Huru Staff:

Send us your articles, questions, feedback, suggestions, press releases and all others to Whats app on +255657905751
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post