» » ETHELDREDER KOPPA : Mwanamke anayetamba katika sekta ya ujenzi

ILI UPATE HABARI ZETU KWA URAHISI BOFYA HAPA KUINSTAL APPLICATION YA MZALENDO HURU KWENYE SIMU YAKO



Kuna kazi zinachukuliwa kuwa ni za wanaume tu hata inapotokea mwanamke anafanya huonekana mtu wa tofauti.
Etheldreder Trecia Koppa (29), ni moja kati ya mabinti wachache ambao wameonyesha uthubutu kiasi cha kufikia mafanikio ambayo ni nadra kufikiwa hata na wanaume, huku akifaulu katika kazi iliyo mbele yake.
Hatua hiyo imemfanya Ethel afanikiwe kupata tuzo yake ya kwanza akiwa kama meneja wa mipango na ujenzi Afrika mwaka 2016.
Katika mazungumzo yake mapema wiki hii, Koppa ambaye ni Meneja Programu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), anasema tuzo aliyoipata hutolewa kwa wanawake wote ambao wapo katika sekta ya ujenzi Afrika.
“Lilikuja tangazo, bosi wangu akalituma akitaka nishiriki nikajaza fomu akanisainia. Nakumbuka ilikuwa Februari,” anasema.
Anasema awali alijua ameikosa nafasi hiyo, lakini baada ya miezi miwili akapigiwa simu na kupata taarifa za kuteuliwa. “Wakanitumia kila kitu ili niweze kushiriki katika hafla ya utoaji tuzo, nikashinda,” anasema.
Ethel anasema ili kupata nafasi hiyo mhusika anatakiwa kuwasilisha wasifu wake japokuwa pia wanangalia elimu, miradi gani amefanya na mchango wake katika tasnia.
Akielezea elimu yake anasema alihitimu Chuo Kikuu cha Ardhi shahada ya kwanza na kufanya kazi kwa mwaka mmoja katika kampuni ya CQS Services na baadaye alipata fursa ya kujiendeleza kielimu ambayo alikwenda kusoma shahada ya Uzamili Chuo Kikuu cha Heriot Watt.
“Nilipohitimu nilipata kazi hapa shirika la nyumba, Machi 2014 kama Meneja Programu Msaidizi.”
Katika ufanisi wake kuna changamoto nyingi anakutana nazo kama binti: “Fani hii ni ya wanaume bado wanawake hawana mwamko, ninapambana sana kitu cha kwanza unatakiwa kujiamini wewe na timu yako, unakuta katika timu nzima mwanamke uko peke yako na wewe ndiyo Project Manager.”
“Hivyo unawajibika katika kila kitu, unatakiwa kujiamini ili ukamilishe kazi na unatakiwa kujijenga kisaikolojia na vyovyote unavyojiwekea ndiyo matokeo ya baadaye, hiyo ndiyo changamoto kubwa, vingine vyote ni vitu vidogo vidogo kwa hiyo kila siku ninajifunza na nakutana na vitu vipya kila siku,” anasema Ethel.
Anasema kitu cha msingi anachokifanya ni kusoma kila siku ili kujua mambo mengi, huku akijitahidi kuwa mwenye uharaka zaidi.
“Najua mimi bado ni mchanga sana katika fani kwa hivyo ninatakiwa kujijenga zaidi ili niweze kufanya kazi yangu vizuri.”
Anasema bado watu hawaamini mwanamke akipewa nafasi, anasema wengi wanafikiri kwamba huenda kila nafasi ambayo mwanamke ameifikia basi ni kwa upendeleo.
“Hata niliposhinda hii tuzo, hongera hazikuwa nyingi wengi waliuliza kwanini umeshinda ilikuwaje, kitu cha kwanza watakachokuuliza he umepata hiyo tuzo nani amekupeleka huko yaani hawaamini kama naweza kusimama mwenyewe,” anasema Ethel.
Akitoa wito kwa wanawake, Ethel anasema kitu cha kwanza wanatakiwa kufanya kazi kwa bidii pia wanatakiwa kujiamini, haiwezekani wapewe nafasi kisha wakaharibu bali wanatakiwa kufanya kazi kwa bidii ili kufikia malengo na hata kuonyesha kwamba wanaweza.
Akielezea malengo yake anasema anataka kuwa Project Manager ambaye ataweza kufanya kazi sehemu yoyote duniani, “ninajua nikitimiza miezi tisa nitaweza kuingia huko ili nipate kibali cha kuweza kufanya kazi popote ambacho kinapatikana Marekani pekee.”
Hata hivyo, anasema ili afanikiwe kufika huko anatakiwa kuwa amefanya kazi miaka mitatu, awe na shahada ya uzamili ambayo tayari anayo lakini pia kuna mitihani anatakiwa kufanya.
Anasema hili kufikia ndoto za wanawake wengi inapaswa kuwapo idara ambayo itashughulika na masuala ya wanawake pekee.
Akielezea kilichomvutia kusomea fani ya ujenzi, Ethel anasema alipoingia Chuo Kikuu cha Ardhi haikuwa mpango wake wa awali kwani alihitaji kusomea masuala ya madawa.
Anasema mama yake alimwona akifanya kazi za kukaa ofisini kitendo ambacho hakupendezewa nacho, alipohitmu kidato cha sita mama yake alimshauri.
“Aliniambia kuna masomo ya ujenzi najua yatakufaa, nikaingia na kuanza kuangalia hiki na hiki mtandaoni kabla sijaomba kujiunga, nilipoanza masomo haikuwa vigumu kwangu,” anasema.
Uhusiano
Kama ilivyo kwa mabinti wengine, Ethel ana hisia za kimapenzi. Lakini katika maisha yake anasema hataki kuharakishia mambo. Hasa linapokuja suala la kuolewa.
“Unahitaji muda wa kukaa sawa, lazima ujitambue kuanzia muda wa kumaliza chuo, ujipe muda wa kujijenga, ndoa ni kitu kizuri lakini hakihitaji haraka,” anasema Ethel.
Anasema tangu amalize chuo miaka takribani mitatu iliyopita amekuwa ni mtu mwenye utofauti sana.
“Kuna watu wananishangaa, ninaamini kwamba ndoa ni nzuri, lakini kabla hujaikimbilia inahitaji uwe umekaa na kujitafakari uweze pia kujitambua,” anasema.
Anasema msichana kujipa muda wa kujijenga inamsaidia kuwa na msimamo katika maisha kwani hata atakaposhindwa katika baadhi ya mambo anakuwa na udhubutu, “nimelelewa na mama yangu pekee, kwa hiyo najua unahitaji kuwa jasiri yaani mkakamavu na unajijua kwamba kesho likitokea la kutokea na nikabaki peke yangu unaweza kutengeneza familia nzuri pia inakupa ulinzi.”
Ethel anasema tayari yupo katika uhusiano wa kimapenzi, “ninaye lakini huwa sipendi kuulazimisha uhusiano, kwa kuwa watu wananiambia kwmaba kwa sababu klwa sasa umefanikiwa kuwa hivi unahitaji kuolewa, lakini kwangu mimi sivyo si kitu cha kulazimisha, kama ikitokea itatokea kila mmoja aamue kwa wakati wake.”
ILI UPATE HABARI ZETU KWA URAHISI BOFYA HAPA KUINSTAL APPLICATION YA MZALENDO HURU KWENYE SIMU YAKO

About Mashak

About Mzalendo Huru Staff:

Send us your articles, questions, feedback, suggestions, press releases and all others to Whats app on +255657905751
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post