“Sheria zinazohusu masuala ya Usalama barabarani inabidi zifanyiwe marekebisho ili ziweze kusaidia kupunguza vifo na majeruhi kwani zilivyo sasa hazitoi adhabu kali kwa wanaokiuka sheria hizo”alisema Kamanda Mpinga.
Aidha Kamanda huyo alisisitiza kuwa suala la Usalama Barabarani ni la kila mmoja hivyo inabidi litiwe mkazo na watu wote. Kwa upande wake Mkurugenzi wa TAWLA, Bi Tike Mwambipile amesema chama hicho kwa kuzingatia umuhimu wa kushughulikia masuala ya Usalama Barabarani kimeona ni vyema kikafanya kikao hicho ili kupata mawazo ya wadau.
Bi Mwambipile amesema vifo vingi vinavyotokana na ajali za barabarani vinawaacha wanawake wengi wakiwa wajane na watoto yatima wanaongezeka.
Ameongeza kuwa fedha nyingi zinatumika kuwahudumia majeruhi badala ya kufanya shughuli nyingine za maendeleo ya jamii.
Naye Mwenyekiti wa TAWLA, Bi Aisha Bade amesema mabadiliko makubwa ya sera na sheria za usalama barabarani ni lazima yafanyike ili kupunguza athari zitokanazo na ajali za barabarani.
Bi Bade amesema TAWLA kwa kushirikiana na wadau wengine inafanya juhudi za makusudi ili kuhakikisha sheria hizi zinabadilishwa ili kukabiliana na janga hili.
Visababishi vya ajali kwa hapa nchini vimetajwa na Mratibu wa Mradi Bloomberg wa Usalama Barabarani, Bi Mary Kessy kuwa ni ulevi, kutofunga mkanda, kutoweka vizuizi vya watoto kwenye magari, mwendo kasi na kutovaa kofia ngumu kwa waendesha pikipiki.
