Dar es Salaam. Mtu mmoja anadaiwa kufariki dunia usiku huu baada ya kugongwa na basi la mwendokasi, eneo la Kariakoo.
Hata hivyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Lucas Mkondya licha ya kuthibitisha kutokea kwa ajali hiyo, amesema chanzo na athari havijafahamika kwa sababu askari wapo eneo la tukio hivi sasa.
Shuhuda wa tukio hilo ameeleza kuwa, basi hilo limemgonga mtu inayedaiwa kuwa alikuwa mlemavu ambaye alikuwa amelala pembeni mwa barabara ya mabasi hayo eneo la Congo, wakati basi hilo lilipokuwa likimkwepa mwendesha pikipiki aliyeingia kwenye barabara hiyo ghafla wakati taa za makutano ya Uhuru na Msimbazi zikiwa zimeruhusu.
Alilieleza Mwananchi kuwa baada ya kumkwepa mwendesha pikipiki, dereva wa basi alimgonga mtu huyo na kutenganisha baadhi ya viungo vyake na kiwiliwili.
